Wednesday, October 10, 2007

Nani alijua Kapuya anamiliki mgodi wa madini?

Nkuzi Mhango Nkwazi

KWANZA nampa pole Profesa Juma Kapuya (pichani), Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, kwa ajali iliyompata.

Hata hivyo binafsi napenda kusema wazi kwamba Oktoba 3 nilifumbuka macho baada ya vyombo vya habari kuripoti kuwa Waziri Juma Kapuya aliibwa mali fulani. Viliendelea kuelezea kuwa wizi huo ulitokea huko Longido kwenye mgodi wake wa rubi.

Binafsi nilishtuka kusikia kuwa kumbe Kapuya ni milionea anayemilki mgodi. Japo sheria zetu hazizuii waziri kuwa na mali, kuna maswali yalijitokeza kutokana na taarifa hii inayoweza kuonekana ya kawaida.

Swali la kwanza, je, Waziri Kapuya alipataje mgodi huu hata bila kuwapo matangazo? Je, ni mawaziri au vigogo wengine wangapi kama yeye wanaomilki migodi hata mali nyingine kimsingi zinazopaswa kujulikana zilivyopatikana?

Je, hii inaweza kuwa ndiyo staili ya watawala wetu kutumia uwekezaji na ubinafsishaji kujipatia na kumiliki mali nyingi na za thamani binafsi? Je, aliwezaje kumiliki mgodi iwapo kila siku wachimbaji wetu wadogo wadogo wanatimuliwa?

Je, ni yale yale ya Kiwira? Je, wananchi wanaichukuliaje hii hali wakiangalia jinsi maslahi yao yanavyozidi kuhujumiwa na baadhi ya watawala ama wawekezaji kutokana na kutamalaki kwa rushwa na kulindana hasa kwenye sekta ya madini?

Kwa anayekumbuka tume iliyoundwa na Mzee Benjamin Mkapa kuhusiana na kadhia ya ugomvi baina ya wachimbaji wadogo wadogo na wawekezaji kule Mirerani, atakuwa anakumbuka kulivyozuka tuhuma kuwa mkuu wa zamani wa majeshi ya ulinzi, Jenerali Robert Mboma, hakufaa kuwa mwenyekiti wa tume hiyo kutokana kuwa na vitalu vya madini huko. Uvumi ulikwenda mbali hata kuhusisha maofisa wengine waandamizi wa Serikali ya Awamu ya Tatu na familia zao.

Kutokana na wananchi kuchukulia mambo kijuujuu, kombe lilifunikwa na mwanaharamu akapita. Pia kuna gazeti la kila siku lililowahi kuripoti juu ya hujuma kwa jeshi la wananchi wakati jenereta kubwa ilichukuliwa na kigogo wa jeshi hilo wa zamani, kiasi cha kuwa analitumia kwenye miradi yake binafsi. Tunakumbuka ilikuwa ni gazeti la ‘Tazama’ la mwaka 2004. kutokana na ubabe na ukosefu wa uwazi na uhuru wa kweli wa vyombo vya habari, suala hili nalo liliuawa kimya kimya!

Turejee kwa Kapuya na kumilki mgodi wa rubi.

Kwa mtu anayechambua kila kitu kwa kina, habari kuwa Kapuya anamilki mgodi si ndogo wala ya kawaida. Inaamsha maswali mengi kuliko majibu. Hasa ikizingatiwa kuwa mwezi Septemba kuliripotiwa habari kuwa sekta ya utalii inamilikiwa na vigogo na familia na kampuni zao binafsi. Walitajwa Waziri Muhammed Seif Khatib na kampuni yake, Rashidi Kawawa na wengine wazito.

Hii haikuwa habari nyepesi wala ya kupuuzia bali kungoja kuona mengine yatakayoibuka kama hili la Kapuya na kumiliki mgodi.

Ukiongeza na taarifa za hivi karibuni juu ya kampuni mizengwe na yenye kila aina ya utata ya Tangold na mali na fedha za umma zinamilikiwa na watu binafsi kiasi cha kuweza hata kuruhusiwa kisheria kuhamishia hisa zao kwa wake na watoto zao, unajenga shaka. Ukiunganisha na madudu kama Meremeta na upuuzi mwingine unazidi kuhoji kuhoji na kuhoji bila kupata jibu bali kuzidi kuuliza!

Ukichanganya na ugumu wa watawala kutaja mali zao, unaweza hata kufikia hitimisho kuwa kuna kitu tena kikubwa ambacho kimsingi ni hatari kwa maslahi ya umma.

Kama tulivyoeleza hapo juu kuwa si vibaya wakubwa kumiliki mali. Lakini wanapozifanya kuwa kificho lazima mtu ajiulize inakuwa hivyo kwa kuogopa nini kama siyo jinai nyuma ya upatikanaji wa mali hizo?

Rais Mwai Kibaki na familia yake wana makampuni yapatayo 64. Makamu wa Rais Moody Arthur Awori na familia yake wana viwanda. Kila Mkenya anajua hivyo na hana shaka wala pingamizi. Lakini inapokuja kwetu ambako ukweli ni kwamba tulikuwa wajamaa jana, maswali na mashaka yanakuwa mengi.

Je, hawa wanaotuaminisha kuwa uwekezaji na ubinafsishaji unalipa ni kwa sababu wamejihudumia wao kwanza? Unalipa kwao au kwetu? Je, hii haiwezi kuathiri maslahi ya umma inapotokea kukawa na mgongano wa kimaslahi baina ya mali hizi na za umma?

Juzi juzi ulitoka uvumi kuwa Benki ya M ni ya Mkapa. Waliokanusha walikanusha na umma ukanyamaza! Waliokanusha hata hivyo walituachia faida kuwa Benki ya M ni mpangaji kwenye jumba la Mkapa.

Hapo maswali ndipo yaliopanza kujengeka. Je, Mkapa alijenga lini jumba hilo? Alikuwa ameliorodhesha kwenye mali zake alizotangaza wakati wa mkwara wa kutangaza mali? Alilipata alipoingia madarakani kwa kutumia urais? Je, ana majumba mengine mangapi kama haya? Kwa nini ayapate kisirisiri? Kuna nini hapa? Je, ni mawaziri na maofisa wengine wa serikali wana majumba hata mahoteli ambayo umma hauyajui ili upime kama yanalingana na mishahara yao? Je, wanaficha kwanini?

Kuna haja ya serikali kukubali haraka maofisa watangaze mali zao umma uzijue kuepusha kutumia uficho huu kutuibia wakijinufaisha sisi tukiendelea kuteseka. Pia kuna haja ya kubadili katiba yetu itamke wazi kuwa tunajenga taifa la kichuuzi badala ya kijamaa. Maana mtu anaweza akatoka siku moja akataka hizi mali za kificho zitaifishwe kwa sababu nchi ya kijamaa hairuhusu watendaji wake kujilimbikizia mali.

Umma ungetaka kujua licha ya jinsi walivyopata mali hizi, kama mali zao zinaingiliana na shughuli zao za kiserikali. Kwa mfano, mhusika huwa anatembelea zilipo mali yake kwa gharama za serikali? Je, kuna miundombinu kama barabara hata visima vya maji alivyoelekeza huko kutokana na kuwapo mali zake? Je kuna magari au vitendea kazi hata watumishi wa umma vilivyopo au waliopo chini yake anavitumia kwenye miradi yake? Na mambo mengine kama hayo.

Umma ungetaka kujibu maswali haya. Maana wahusika ni binadamu sawa na wengine. Mfano mmoja rahisi ni nchini Kenya. Rais Kibaki alipoingia madarakani alitoa tenda ya kujenga barabara kwenda kwenye jimbo lake. Hii ilichukuliwa na Wakenya kama kujihudumia kwa mgongo wa umma.

Hata nchini mwetu kuna waziri mmoja kutoka mkoa mmoja wa kaskazini aliyeshutumiwa kupeleka umeme milimani kwao kwa sababu tu alikuwa anatokea huko na hii ilimsaidia kuchaguliwa mbunge wa eneo hili kwa muda mrefu.

Lakini alifanya yote kwa kuwahujumu wengine. Hata kuna baadhi ya mikoa, wilaya hata majimbo ya uchaguzi yamepewa hadhi yake kutokana na kujuana au kulinda nafasi za watu kisiasa. Hivyo kama hali hii inaweza kufanyika hata kwenye mambo ya siasa, inakuwaje kwenye miradi ya wakubwa? Je, hii ni mojawapo ya usiri unaozunguka mali za watawala wetu?

Je, hawa wanaposema ubinafsishaji una manufaa kwa taifa tuwaamini kwa vile wamefanikiwa wao wakati sisi tunaendelea kuangamia? Je, huu si ubinafsi na ufisi unaopewa jina zuri la ubinafsishaji na urekebishaji wa mashirika ya umma?

Kapuya na wengine kama hawa watoe maelezo. Vyombo vya habari vianze kuziwinda mali za namna hii na kuzianika. Pia wananchi wasiwe wanachukulia kwa wepesi au ukawaida habari kama hizi ambazo zina maslahi kwao.

nkwazigatsha@yahoo.com /Tanzania daima

2 comments:

ARO GERALDES said...

May be, you can't read my blog in Spanish, but I'm an african football fan. I'm come here lloking for information about Taifa Star.
Best regards from Argentina!
Pablo
www.arogeraldes.com

Chama Cha Watanzania Oslo - CCW Oslo said...

Hi Pablo

Thanks a lot for visiting Tanzanian Association Oslo´s blog. About Taifa Stars look at Tanzania Football Federation website:

http://www.tfftanzania.com/

About African football in general look at

http://www.cafonline50.com/

Thanks again for visiting our blog.

Your blogmaster.