Saturday, July 18, 2009

Mbunge aponda miswada

bungeni kuwa ya `Kizungu



Ramadhan Mbwaduke


Mbunge wa Kigoma Kusini Mheshimiwa Manju Msambya, amesema haina maana yoyote kuendeleza utamaduni wa kuandaa miswaada ya kuwasilisha Bungeni kwa lugha ya Kiingereza ilhali waijadili kwa Kiswahili.

Amesema hiyo ni dalili ya wazi kuwa kuna hulka ya kuthamini zaidi lugha ya kigeni.

“Miswaada inaandikwa Kiingereza, halafu sisi (wabunge) tuinaijadili Kiswahili... kwanini? Ni vyema tukaienzi lugha yetu kwa kuandaa miswaada hii kwa Kiswahili kwani hata wananchi wetu wengi wanaelewa lugha hii,” akasema Mheshimiwa Msambya wakati akichangia mjadala wa makadirio ya bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo.

Aliongeza kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuheshimu lugha ya Kiswahili na kuipa hadhi yake, kwani hata mataifa mengine yaliyoendelea duniani yamefikia mahala walipo sasa kiuchumi kwa sababu wanaheshimu lugha yao na kuitumia kufundishia shuleni na vyuoni kwa namna inayoeleweka zaidi.

Akasema nchi kama za Korea Kaskazini na Kusini, Ujerumani , China , Italia, Urusi na nyinginezo nyingi hutumia lugha zao katika kufundisha na wala si Kiingereza, lakini bado zimeweza kufanikiwa.

ALASIRI


No comments: