Thursday, February 02, 2012

Serikali kutengeneza hati mpya za kusafiria


NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Balozi Khamisi Kagasheki, amesema serikali imeanza mchakato wa kutengeneza hati mpya za kusafiria ambazo haziwezi kughushiwa.

Kauli hiyo aliitoa bungeni jana alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Magu, Festus Limbu (CCM), aliyetaka kujua mkakati uliopo serikalini katika kuzuia vijana wanaosafiri nje ya nchi kwa kutumia hati za kughushi.

Balozi Kagasheki alisema licha ya kuwepo kwa baadhi ya vijana wanaotumia hati za kusafiria za kughushi lakini wapo wanaosafiri bila hata hati hizo.

Alidai kuwa vijana wengi wanazamia na kwenda nje ya nchi kwa malengo ya kusaka maisha bora na pindi wanapobainika hurejeshwa nchini.

Alisema kutokana na hali hiyo, serikali ipo katika mchakato wa kuhakikisha inatengeneza hati ambazo haziwezi kughushiwa ikiwamo kuanza kutengeneza vitambulisho vya kitaifa.
Alifafanua kuwa baada kumalizika kutengeneza vitambulisho vya kitaifa, itasaidia kubaini kuwapo kwa watu ambao si Watanzania na kuwarejesha makwao.

Kutoka gazeti la Tanzania Daima

No comments: