Friday, April 06, 2012

Bingu wa Mutharika afariki dunia

Rais wa Malawi Bingu wa amefariki dunia baada ya kupatwa na mshtuko wa moyo, akiwa na miaka 78. Duru kutoka kwa serikali zimethibitisha kifo hicho kwa BBC. Mwili wa wa kiongozi huyo umepelekwa Afrika Kusini. Hata hivyo serikali haijatoa taarifa rasmi kuhusu kifo cha Wa-Mutharika. Mmoja wa madaktari waliokuwa wakimhudumia kiongozi huyo ameambia BBC, Wa-Mutharika alikufa baada ya moyo wake kusimama.

Wadadisi wameonya kifo cha rais huyo huenda kikazua mgogoro wa uwongozi. Katiba ya nchi inampa nafasi Makamu wa Rais kuongoza nchi endapo Rais atafariki au kuugua kiasi cha kushindwa kuongoza taifa.Hata hivyo Makamu wa Rais nchini Malawi, Joyce Banda alitofautiana na Wa-Mutharika kufuatia mzozo wa urithi wa uongozi ambapo alifukuzwa kutoka chama tawala,Democratic People's Party (DPP).

Kakake rais ambaye ni Waziri wa mambo ya nje Peter Mutharika aliteuliwa kugombea urais hapo mwaka wa 2014.Mwandishi wa BBC mjini Blantyre Raphale Tenthani amesema mawaziri wamekuwa na kikao usiku mzima kujadili hali ya sasa. Rubaa za serikali zimenukuliwa zikisema kwamba maiti ya Rais imesafirishwa Afrika Kusini huku maafisa wakitafakari hali ya sasa.

Bingu wa Mutharika aliingia madarakani mwaka wa 2004. Baadaye alikihama chama chake cha United Democratic Front (UDF) kwa tuhuma za wanachama kuhujumu harakati za kupambana na ufisadi. Alichaguliwa tena mwaka 2009, lakini katika siku za karibuni wakosoaji wake wamemlaumu kwa kuegemea sera za kiimla.

Rais huyo alikumbwa na shinikizo za kuachia madaraka kwa tuhuma za kupendelea ukoo wake, na kuharibu madaraka.Wa Mutharika aliwakera wafadhili wa kigeni hasa baada ya kumfukuza balozi wa Uingereza Fergus Cochrane-Dyet, na kufanya utawala wa Uingereza kusimamisha msaada kwa Malawi.


No comments: