Tuesday, April 17, 2012

Kocha wa zamani wa Taifa Stars, Marcio Maximo akutana na Rais Jakaya Kikwete na mama Salma Kikwete mjini Sao Paulo Brazil


Kocha wa zamani wa Taifa Stars Marcio Maximo akimpa Rais Jakaya Mrisho Kikwete zawadi ya jezi ya timu ya Democrata anayofundisha nchini Brazil alipokwenda kumsalimia Rais katika hoteli ya Tivoli jijini Sao Paulo.

Kocha wa zamani wa Taifa Stars Marcio Maximo akisalimiana na  Rais Jakaya Mrisho Kikwete   alipokwenda kumsalimia Rais katika hoteli ya Tivoli jijini Sao Paulo.

Kocha wa zamani wa Taifa Stars Marcio Maximo akimsalimu mke wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Mama Salma Kikwete alipokwenda kuwasalimia  katika hoteli ya Tivoli jijini Sao Paulo.Picha na IKULU


Na Anna Nkinda – Sao Paul, Brazil

18/04/2012 

Vilabu vya soka nchini vimeshauriwa kuwa na timu nzuri kuanzia ngazi ya watoto wenye umri wa miaka nane, vijana  na kuendelea ili kupata timu bora ya Taifa.

Wito huo umetolewa na aliyekuwa kocha mkuu wa timu ya Taifa Star  Marcio Maximo wakati akiongea na waandishi wa habari mjini Sao Paul.

Maximo alisema kuwa timu nyingi ambazo ni bora na zinafanya vizuri katika mchezo wa soka zimekuwa zikiwaandaa watoto wenye vipaji vya mchezo huo wangali wadogo ili waweze kuwa wachezaji wazuri hapo baadaye.

Kocha Maximo pia alikutana na kufanya mazungumzo na Rais Jakaya Mrisho kikwete, ambapo alimnshukuru sana Rais kwa ushirikiano wa hali ya juu aliompa wakati alipokuwa akiifundisha Taifa Stars miaka takriban mitatu iliyopita.

Kwa upande wake Rais Kikwete alimpongeza Kocha Maximo kwa juhudi zake za kuendeleza soka la Tanzania, akimwambia uwepo kwake Tanzania kuliasidia sana kuiweka nchi katika ramani ya mchezo huo.

Rais Kikwete alikubaliana na kocha huyo kwamba ili timu ya Taifa ifanye vyema ni lazima maandalizi yaanzie ngazi za chini, ikiwemo vilabu kuwa na timu za watoto na vijana ambao baadaye watakuwa hazina ya Taifa Stars.

Kuhusiana na uvumi ulioenea kuwa anataka  kwenda kufundisha timu za Taifa Stars, Azam na Yanga alisema kuwa siyo kweli na wala hajawasiliana na timu hizo na hawezi kwenda kufundisha  kwani hivi sasa anamkataba wa kufundisha timu ya Democrata iliyopo nchini humo.

Rais alimshukuru Kocha Maximo kwa kuja kumsalimia na kumpa zawadi ya jezi ya timu ya Democrata anayofundisha, na kumtakia heri na fanaka katika kazi yake hiyo.

 “Timu ya Taifa Star ina kocha mzuri ambaye ninamuheshimu na ninaukubali ufundishaji wake hivyo basi kupitia kocha huyo ninaamini watanzania watazidi kuendelea katika soka na kufika mbali zaidi”, alisema. 

Maximo alimalizia kwa kusema kuwa  anamawasiliano mazuri na watanzania na anawapenda ndiyo maana kila mahali anapopita anajivuna na kusema  kuwa Tanzania ni nchi yake ya pili.

Hivi sasa Maximo ni kocha wa timu ya  Democrata iliyopo nchini humo ambapo wiki ijayo inatarajia kuanza mashindano ya taifa yatakayopelekea kupata wachezaji bora watakaoshiriki mashindano ya kombe la Dunia yanayotarajia kufanyika mwaka 2014 nchini Brazil.

No comments: