Wednesday, August 29, 2012


Neno la usiku:
CCM na sifa ya mchawi!


Ndugu zangu,

Usiku wa saa sita  umeingia tena hapa Iringa. Kabla sijaondoka kwenye meza ya kibarua changu nina neno fupi la usiku.

Naam, inasemwa, kuwa mchawi mchukie, lakini, sifa yake mpe, anajua kuroga!

Majuzi hapa nilipokuwa kwenye shughuli za kijamii kijijini Mahango, Madibira, kuna kitu kilichonifanya nishangae, lakini, baada ya tafakuri nikauona ubunifu kwa aliyekitenda.

Nikiri, kuwa huko nyuma  nimefanya vikao kadhaa na Kamati ya Shule ya Mahango chini ya Uenyekiti wa Bw. Victor Kadama ( Pichani).  Sikupata kujua kuwa Victor Kadama, mbali ya kuwa Mwenyekiti wa kamati ya Shule, pia ni Katibu Mwenezi wa CCM, Kata ya Madibira. Ndio, Victor Kadama ndiye Nape Nnauye wa Madibira. 

Maana, kwenye vikao vyetu hakuwahi hata siku moja kuvaa nguo za rangi ya chama chake wala kofia. Lakini, majuzi hapa tulipokuwa na mkusanyiko mkubwa wa wanakijiji kuwapokea wageni kutoka Norwich, Uingereza  waliokuja  kuzindua mradi wa ujenzi wa Maktaba ya Kijamii kijijini hapo, basi, kwa siku mbili mfululizo, nilimwona Bw. Victor Kadama akiwa ametinga kofia ya chama chake, CCM.

Bw. Kadama  kwa siku zote mbili hakuongea hata neno moja kuhusu chama chake, lakini, kofia yake ilikuwa inaongea.  Kulikuwa na uwepo wa CCM kupitia kwa kofia ya Kadama. Na hata  wageni waipopangiwa ziara ya miguu kuona mazingira ya kijiji, Victor Kadama na kofia yake haraka alichukua jukumu la kuongoza msafara.  Aliendelea kufanya ' kazi ya uenezi' wa Chama chake.

Kwa vyama vingine vya siasa kuna ya kujifunza kutoka kwa CCM. Pamoja na dhambi zao zote, CCM bado wana oganaizesheni inayoeleweka na  yenye kufikia hadi ngazi za vitongoji. Ni mtaji wao mkubwa kisiasa. Tofauti na vyama vingine, makada wa CCM wanajipenyeza kila mahali, iwe kwenye kamati za shule au za kuchimba visima. Ndio, hata, uwe na harusi ya mwanao, bado kuna makada wa  CCM watakaojipenyeza kwenye Kamati za harusi.

Naam, mchawi mchukie, lakini sifa yake mpe, anajua kuroga, hakyamungu!

Maggid,
Iringa.
0788 111 765

No comments: