Wednesday, October 31, 2012

Polisi wadaiwa kufanya unyama Zanzibar


MTU moja mkazi wa Mkele jana alinusurika kuuawa katika msako wa kuwakamata watu wanaotuhumiwa kusababisha vurugu zilizotokea wiki moja iliyopita mjini Zanzibar.

Vurugu hizo ziliibuka Oktoba 17 mwaka huu baada ya kiongozi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu (JUMUIKI) Sheikh Farid Ahmed Hadi kutoweka katika mazingira ya kutatanisha Oktoba 16, mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa bahari mjini hapa jana, kijana aliyenusurika kuuawa, Salum Bakari Muya alidai aliteswa kwa kukatwa ngozi kwa kisu kichwani na kasha kunyonyolewa nywele polisi ambao pia walikuwa na silaha.

Alisema kabla ya kukutwa na tukio hilo alikuwa amekaa na wenzake wakiwa wanasubiri tenda ya mizigo ya kusafirisha kwa kutumia magari ya punda.

“Nilikuwa nabangaya – yaani kubangaiza –wakatokea polisi sita, walipofika nilipokaa wakanifunua kofia na kunikata kipande cha ngozi na nywele kichwani kwa kisu,” alisema Salum.

Alidai polisi waliomfanyia ukatili huo ni wa kikosi cha FFU na kwamba baada ya kitendo hicho waliamua kumpeleka kituo cha afya cha JKU kilichopoa Saateni kwa matibabu ya awali.

Salum alidai kuwa baada ya kupata matibabu katika kituo hicho cha JKU iliamriwa kwamba apelekwe Hospitali Kuu ya Mnazimoja kwa vile alikuwa anavuja damu nyingi.

Hata hivyo alisema alishangaa kabla ya kufika Mnazimoja polisi hao waliamua kumtekeleza katika eneo la kwa Abbas Hussein, kilometa chache kutoka walipomtoa hospitali ya JKU.

“Hawakunifikisha Manazimoja, wakaniacha na kuondoka huku wakisema ubaya ubaya mtakoma waambie na wenzio,” alisimulia Salum akiwa na bandeji aliyofungwa wakati anapata huduma ya kwanza.

Alisema baada ya kutelekezwa na polisi aliamua kwenda Welesi huko Kikwajini kwa lengo la kuzungumza na waandishi wa habari juu ya mkasa uliompata.

Baada ya kusimulia mkasa huo, Salum ambaye alifuatana na kaka zake walioomba wasiandikwe majina baadae alipelekwa hospitalini kwa matibabu zaidi.

Alipoulizwa juu ya tukio hilo, Kamishana wa Polisi Zanzibar, Mussa Ali Mussa alisema bado hajapopewa taarifa na kwamba iwapo mwathirika atalalamika kituoni polisi watachukua hatua ya kucunguza.

“Tumezoea kulalamikiwa, kama mtu amefanyiwa ukatili kwanini asiripoti kituo cha polisi, hapo ujue kuna jambo anaficha,” alisema Kamishna Mussa.

Lakini baada ya kuelezwa na mwamdishi wa habari hizi kwamba kijana huyo amepelekwa hospitali na kaka zake, Mussa alisema aliahidi kufuatilia tukio hilo

Kitendo cha Salum kufanyiwa ukatili na watu wanaodaiwa kuwa polisi kimetanguliwa na matukio ya vijana wenguine wawili kuuawa wakati wa utekelezaji wa zoezi la msako huo mjini Zanzibar mwezi Oktoba mwaka huu.

Imedaiwa kuwa Hamad Ali Kaimu aliuawa Ijumaa iliyopitama wakati akiwa mikononi kuwa polisi katika eneo la Magomeni na Salum Hassan Mahanju alikufa baada ya kupigwa risasi katika maeneo ya Amani Fresh na watu waliotajwa kuwa maofisa ulinzi na usalama.

Mbali na vijana hao, askari mmoja Koplo Said Abdulrahman aliuawa na watu wasiojulikana huko Bububu baada ya tukio la kutoweka Sheikh Farid.

Tokea kuanza kwa vurugu hapa Zanzibar jumla ya watu watatu wamefariki ikiwa mmoja ameuwa na watu wenye hasira huku jeshi la polisi likidaiwa kuwauwa vijana wawili hali sio shuwari kufuatia unyanyasaji na ukiukwaji wa haki za binadamu unaodaiwa kufanywa na jeshi la polisi kwa kisingizio cha kuwatafuta wahahalifu.Wakati jeshi la Polisi visiwani Zanzibar likiendelea kuwasaka wahalifu, baadhi ya wananchi wamejitokeza kulalamikia juu ya operesheni hiyo ikiwemo ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na jeshi hilo uliosababisha kifo cha kijana mmoja akiwa mikononi mwa polisi.

Chanzo: Voice of Zanzibar on Facebook

No comments: