Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais,
Fatma Abdulhabib Ferej.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), imesema
Zanzibar imegeuzwa kituo cha kuingiza na kusafarisha dawa za kulevya nje ya
nchi.
Kauli
hiyo ilitolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, Fatma
Abdulhabib Ferej, wakati akijibu maswali ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi
kwenye kikao chake Chukwani mjini hapa.
Alisema
badala ya dawa za kulevya kusafirishwa kutoka nje kuingizwa Zanzibar, badala
yake zimekuwa zikitoka Zanzibar kwenda nje ya nchi.
Hata
hivyo, alisema serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwamo kuwakamata
watu kadhaa na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria.
Aidha,
Waziri Fatma Ferej, alifafanua kuwa biashara ya dawa za kulevya hufanyika kwa
usiri mkubwa.
Alivitaka
vyombo vya ulinzi na usalama kuendelea kuchukua juhudi mbalimbali za kupambana
na tatizo hilo.
“Serikali
inazo taarifa kuwa Zanzibar imegeuzwa kuwa kituo cha kupitisha na kusafirisha
dawa za kulevya nje ya nchi, kuna watu wamekamatwa katika Uwanja wa Ndege wa
Zanzibar,” alisema Fatma Ferej.
Alisema
takwimu zinaonyesha kuwa watumiaji wa dawa za kulevya ndiyo wanaongoza kwa
maambukizi ya Ukimwi, hasa wanaotumia njia za kujidunga sindano.
Alisema
idadi ya watu wanaoishi na VVU imekuwa ikiongezeka kutoka watu 5,935 hadi 6,793
mwaka 2012/2013.
“Mheshimiwa
Spika, ni kweli dawa za kulevya ni chanzo za vijana wengi kuathirika na Virusi
vya Ukimwi, na mpango wa kuwafichua wauza unga na wasafirishaji kutoka ndani na
nje ya nchi, upo kisheria,” alisema.
Hata
hivyo, alisema utaratibu wa kuitisha kura ya maoni ya wauza dawa za kulevya,
unaweza kutumika ingawa utekelezaji wake si rahisi kwa kuwa zoezi hilo
linahitaji gharama kubwa kabla wananchi wote kushiriki kupiga kura.
Alisema
Sheria ya Kuzuia Usafirishaji na Matumizi ya Dawa za Kulevya namba 9 ya mwaka
2009, imeweka mpango mzuri wa kuwafichua watu wanaofanya biashara hiyo na mtu
yeyote atakayetoa taarifa atazawadiwa.
Machi
16, mwaka huu, kitengo cha kuzuia dawa za kulevya Zanzibar, kilifanikiwa
kumkamata Alex Vasileios (24), raia wa Ugiriki, akiwa na kilo tano za dawa za
kulevya katika begi akisafiri kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Zanzibar
kwenda nchini Italia.
Mtuhumiwa
huyo alifikishwa mahakamani pamoja na Yusuph Abeid, mkazi wa Zanzibar na
kusomewa mashitaka ya kuingiza dawa za kulevya na kusafirisha kinyume na Sheria
za Zanzibar.
Chanzo:
Nipashe
No comments:
Post a Comment