Tuesday, July 30, 2013

Reginald Mengi - Nchi inanuka rushwa!



MWENYEKITI wa kampuni za IPP, Reginald Mengi ametoboa siri kuwa hakuna mfanyabiashara wa Tanzania aliyefanikiwa katika biashara kubwa kwa kusaidiwa na serikali bila ya kutoa rushwa.

Mfanyabiashara huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (MOAT), alisema yeye aligoma kutoa rushwa kwa watendaji wa serikali jambo lililosababisha kupoteza fursa nyingi ambazo zingemfanya awe na maendeleo zaidi ya aliyonayo hivi sasa.

Kauli hiyo aliitoa jana jijini Dar es Salaam wakati akichangia mada katika uzinduzi wa ripoti ya uchumi na maendeleo barani Afrika kwa mwaka 2013, uzinduzi uliofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Diplomasia.

Alisema kutokanana na kukithiri huko kwa rushwa, maendeleo ya kibiashara na kijamii hapa nchini hayawezi kufikiwa kama jitihada za kupambana na rushwa zitapuuzwa.

“Ili ufanikiwe ni lazima uione fursa iliyopo, lakini tatizo liko wapi mnajua… ni kwa hawa waliopewa dhamana ya kutoa vibali kuendekeza rushwa,” alisema Mengi.

Alisema ni vigumu katika nchi iliyojaa rushwa kuzungumzia suala la amani wakati wananchi wanapata huduma mbovu kutokana na watendaji wa serikali, taasisi na idara zake kuendekeza rushwa.

Alibainisha kuwa idara nyingi za serikali hivi sasa zimegubikwa kwa rushwa kiasi cha kuathiri huduma mbalimbali zitolewazo huku akitolea mfano wa matumizi ya bajeti ya serikali ya sh trilioni 18 yaliyoidhinishwa na Bunge hivi karibuni.

“Tunaweza kuangalia dhamira nzuri ya serikali hasa katika bajeti ya trilioni 18, manunuzi ya umma ni asilimia 80. Kati ya hizo asilimia 20 -30 zinaweza kuishia katika mianya ya wizi na rushwa, na mambo haya yanaweza kufanywa na watu wachache huku wengi wakiangamia kwa kukosa huduma muhimu,” alisema.

Alisema mbali na fedha zinazopotea katika manunuzi ya umma, maeneo mengine yanayofanya madudu kwa kiasi kikubwa ni sekta ya bandari, TANESCO na reli ambako alibainisha kuwa wajanja wachache wanatumia fursa walizonazo kujitengenezea mianya ya kufaidi rushwa ya maeneo hayo.

Aliongeza kuwa mianya ya rushwa isipodhibitiwa Mtanzania wa kipato cha chini ataendelea kuumia hata kama kipato chake kitaongezeka.

Alisisitiza kuwa tatizo jingine linalochangia rushwa nchini ni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutokutambuliwa katika katiba pamoja na kunyimwa uwezo wa kuwashitaki watoaji na wapokeaji wakubwa wa rushwa.

Alisema katika kupambana na rushwa nguvu ya TAKUKURU inaishia katika kuwashitaki watuhumiwa wadogo, huku wakubwa wakisubiri uamuzi wa Mwendesha Mashtaka wa Serikali (DPP).

Mengi alisema ana wasiwasi kuwa kwa hali ilivyo sasa kwenye sekta ya madini nchini hakuna Mtanzania atakayebaki miaka michache ijayo iwapo mambo hayatabadilishwa.

Alibainisha kuwa sera na kauli zinazotolewa midomoni mwa viongozi zinaelekeza kumuwezesha Mtanzania katika fursa mbalimbali wakati uhalisia wa matendo yao hauendani.

“Viongozi wanasema mdomoni kuwa wanataka kuwawezesha Watanzania, lakini ukweli ni kwamba kuna mkakati wa kuwarudisha nyuma kwa kasi kubwa,” alisema Mengi.

Awali, Mwenyekiti wa Shirikisho la Wenye Viwanda (CTI), Felix Mosha akiwasilisha ripoti ya uchumi na maendeleo 2013 kwa bara la Afrika alisema ukosefu wa miundombinu bora katika bara hilo unachangia kwa kiasi kikubwa wawekezaji kushindwa kuwekeza katika maeneo yatakayoweza kumkwamua mwananchi wa kawaida.

Alisema nchi imefanya makosa makubwa kupuuzia kilimo cha kisasa na kukimbilia kuwekeza katika sekta nyingine huku ikiwaacha watu takribani asilimia 80 katika mbio za kuelekea katika mafanikio.

“Tanzania ni miongoni mwa nchi 10 duniani na katika Afrika ni kati ya tano bora ambayo uchumi wake unakuwa kwa kasi kubwa, lakini wananchi wake wanaendelea kuwa katika hali duni. Hii ni kwa kuwa uwekezaji unafanywa katika maeneo yasiyowashirikisha wananchi moja kwa moja,” alisema Mosha.

TANZANIA DAIMA


No comments: