Saturday, July 27, 2013

Amiri jeshi mkuu wa majeshi ya ulinzi na usalama, Rais Jakaya Kikwete ametangaza operesheni kali ya kuwasaka majambazi wanaojihusisha na uhalifu ikiwemo utekaji wa magari na wahamiaji haramu itayoanza wiki mbili zijazo



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameamuru majambazi na wahamiaji haramu wote katika mikoa mitatu nchini kujisalimisha katika muda wa siku 14 kuanzia, Ijumaa, Julai 26, 2013 kabla ya kuanza kwa operesheni kubwa kuliko zote katika historia ya Tanzania nyenye lengo la kukomesha ujambazi katika mikoa hiyo na kukamata wahamiaji haramu.

Rais Kikwete ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu amesema kuwa leo ametoa amri kwa vyombo vyote vya ulinzi na usalama nchini kuanza maandalizii ya operesheni hiyo na hatimaye kuiendesha katika Mikoa ya Kagera, Kigoma na Geita.

“Majambazi wanateka magari, wanaua watu wetu, wanapora mali zao. Watanzania hawawezi kuendelea kuishi kwa hofu, woga na taabu katika nchi yao wenyewe. Tutawasaka majambazi misituni, tutawasaka majumbani, tutachimbua ardhini kutafuta hata silaha zilizofukiwa chini,” amesema Rais Kikwete.

Rais Kikwete ametoa amri hiyo mchana wa jana, Ijumaa, Julai 26, 2013 wakati alipohutubia wananchi wa mjini Biharamulo, Mkoani Kagera, kabla ya kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa barabara ya lami kutoka Kagoma, Wilaya ya Muleba kwenda Lusahuga, Biharamulo.

Rais Kikwete ametoa amri hiyo kufuatia matukio ya mara kwa mara na yasiyokuwa na mwisho ya majambazi kuteka mabasi, kuua watu na kupora mali zadi katika mikoa hiyo, hali ambayo imesababisha malalamiko ya wakazi wa mikoa hiyo.

Rais Kikwete ameaambia wananchi: “Tumeamua kukomesha upuuzi huu katika mikoa ya Kagera, Kigoma Geita. Leo nimetoa maagizo kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama – Jeshi la Wananchi, Jeshi la Polisi, Uhamiaji na Usalama wa Taifa kuandaa operesheni maalum, operesheni kubwa kuliko zote tokea tupate uhuru. Upuuzi huu hauwezi kuendelea.”


No comments: