Monday, August 05, 2013

Uchochoro wa kuvusha dawa za kulevya Dar es Salaam huu hapa



 MFUMO wa ukaguzi wa wasafiri na mizigo yao katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) umetekwa na sasa uko mikononi mwa matajiri na wanasiasa wanaofanya biashara ya dawa za kulevya hapa nchini, MTANZANIA Jumapili linaandika kwa uhakika.

Vyanzo vya habari vya kuaminika vilivyo ndani ya serikali vinavyofanya kazi bega kwa bega na dawati la habari za siasa na uchunguzi la MTANZANIA Jumapili vimedokeza kuwa, baadhi ya watoto wa viongozi wakuu wa nchi, wafanyabiashara wenye ukwasi wa kutisha na wanasiasa wenye utajiri ambao umekuwa ukitiliwa shaka kwa muda mrefu, wamebainika kuingilia mfumo wa kiitelejensia wa JNIA kwa kuupandikizia watu ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa maelekezo yao.

Ripoti ya uchunguzi wa kikachero iliyo mikononi mwa maofisa wa juu serikalini na ambayo waliinukuu katika mazunguzo yao na gazeti hili, inaeleza kuwa mtandao wa matajiri wauza dawa za kulevya umewaondoa wafanyakazi kadhaa watiifu waliokuwa katika kitengo cha ukaguzi wa abiria na mizigo cha JNIA na kupachika watu wao walio kwenye mfumo wa malipo wa wafanyabiashara wa dawa za kulevya.

Sambamba na hilo, walieleza kuwa kitengo cha kupambana na biashara ya dawa za kulevya nchini kimedhoofishwa na hata mbwa wa polisi waliokuwa wakitumika kukagua mizigo ya wasafiri wanaotumia uwanja wa JNIA wameondolewa katika mfumo wa ukaguzi na sasa watumika kwa nadra, hasa zinapovujishwa taarifa za usafirishaji wa dawa za kulevya ambazo hutolewa aghalabu wafanyabiashara hao wanapohitilafiana kibiashara na kuamua kuumbuana.

Taarifa hizi zimethibitishwa na kauli ya Mkurugenzi wa Kitengo cha Kuzuia Dawa za Kulevya, Kamishna Mwandamizi wa Polisi (SACP) Godfrey Nzowa, ambaye katika mahojiano yake na MTANZANIA Jumapili, alieleza kuwa mtandao wa wafanyabiashara wa dawa za kulevya hapa nchini una pesa nyingi zinazouwezesha kufanya jambo lolote ili kufanikisha biashara hiyo.

Kamishina Nzowa, ambaye alitakiwa na gazeti hili kutoa taarifa ya uchunguzi kuhusiana na matukio hayo ya dawa za kulevya, likiwemo lile la Watanzania wawili waliokamatwa nchini Afrika Kusini wakiwa na kiasi kikubwa cha dawa za kulevya pamoja na uwezo wa kitengo chake wa kupambana na wauza dawa za kulevya, alisema kazi hiyo ina changamoto kubwa katika kufanikiwa kwake, kwa sababu inawahusisha watu wenye fedha nyingi hapa nchini.

Alisema, Watanzania wawili, Agnes Gerald (25) na Melisa Edward (24), waliokamatwa na kilo 150 za dawa za kulevya katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo nchini Afrika Kusini, Julai 5, mwaka huu, walifanikiwa kupita JNIA bila kugundulika kutokana na watu waliokuwa kwenye mashine za ukaguzi wa abiria na mizigo.

“Hawa Watanzania waliopita kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere na kukamatwa Afrika Kusini, waliweza kupita kwa sababu inategemea na watu waliokuwepo kwenye mashine za ukaguzi siku hiyo. Unajua hakuna ushirikiano wa karibu baina ya watendaji wanaohusika na udhibiti wa dawa za kulevya. Hilo ni tatizo kubwa linalosababisha vikwazo katika kupambana na mtandao wa dawa hizo.

“Sisi tunategemea kupata taarifa za wauza dawa za kulevya kutoka kwa watu, wakiwemo wakaguzi wa mizigo na abiria, hapo ndipo tunakwenda kumpekua mtu anayeshukiwa kubeba dawa hizo. Tunapopewa taarifa tunafanya ukaguzi, mbwa tunawanusisha, lakini mara chache kwa sababu wakati mwingine wanashindwa kugundua mizigo yenye dawa hizo iliyopuliziwa manukato au kunyunyiziwa kahawa,” alisema Nzowa.

Kamishina Nzowa pia alilalamika kukithiri kwa rushwa kwa watendaji ndani ya kikosi cha kupambana na dawa za kulevya pamoja na jamii kuwa ni jambo ambalo linasababisha kushamiri kwa biashara hiyo.


Chanzo: Mtanzania Jumapili 4.8.2013

No comments: