Wednesday, September 24, 2014

Waziri wa zamani wa CCM, Dr. Antony Diallo amlipua Waziri Mkuu mstahafu Edward Lowassa


Dkt. Antony Diallo.

Tuhuma za Kundi la Makuwadi wa EL dhidi yangu hayana msingi wowote na kama ni kweli Edward amewapa waziseme kwangu na kuhusisha Mheshimiwa Rais ni mwendelezo wa EL kumdharau Rais ambaye alimpa madaraka makubwa na kosa likiwa kukubali ajiudhuru baada ya kufanya madudu aliyoyafanya. Huu ni mwendelezo wa kumsumbus Rais ambao ulianza tangu 2008 baada ya kujiuzulu uwaziri mkuu. Anayoyasema haya sipendi kuyajibu ila kwa ajili ya kuweka kumbukumbu sawa, imebidi niyajibu lakini nikizingatia kuwa sitaweza kuyajibu yale ninayoyajua chini ya kiapo:

Sijamtuma Mzee yeyote kwenda kwa Lowasa kwa sababu sio waziri mkuu tena na hata kama angekuwa bado waziri mkuu nisingeweza kumwambia mtu akaniombee vyeo kwa Lowassa. Hao wazee aliowataja wapo Mwanza na mnaweza kupata namba zao za simu na kuwauliza kama nilishawahi kufanya hivyo. Pili, mwaka 2003/4 haukuwa mwaka wa uchaguzi, ilikuwaje niende kuomba cheo wakati niliingia baraza la Mhe. Rais Mkapa 2001? 

Wakati huo Lowassa hakuwa waziri mkuu! Tatu, mwaka 2004 sijaonana na JK na Karamagi hajanishawishi kumuunga mkono JK mwaka 2005. Mimi ndiye niliyetumwa kumwambia Lowassa asigombee 2005 kwa vile dhambi na tuhuma dhidi yake zilizotolewa na Mwalimu Nyerere zilikuwa kwenye mioyo ya Watanzania na asingeweza kupata kura za ushindi isipokuwa angempunguzia JK kura zake na wote kukosa. Karamagi tumekutana naye bungeni baada ya kuchaguliwa ubunge baada ya kifo cha Mhe. Kinyondo. 

Mimi nimezaliwa na kukua kwa kuzingatia nidhamu ya Kisukuma, sijalelewa kihuni kufika kumsema mtu kama JK. Namsema EL kwa sababu ni mchafu, na sasa sitayasema yaliyo mazito au machafu zaidi dhidi yake, hadi nitakapoona kweli kachukua fomu kugombea Urais! Mimi sijasema Lowassa alidhulumu CCM kupata hisa Vodacom, nilichosema CCM ilikuwa iwe mbia wa MTN, kampuni iliyonyimwa leseni wakijua fika kuwa ilikuwa ikisaidie chama, badala yake wakafanya njama kuvunja tume ya mawasiliano kihuni, na hapohapo wakaipatia vodacom leseni lowasa kwa kutumia watoto wake, alipata walikipata. 

Ushahidi kuhusu hili ni kampuni yake kupewa U-Super Dealer wa Vodacom ambayo uliwafanya wanufaike kwa kuuza simu nchi nzima.
Kama wanasema Lowassa ni mzima, naomba akakimbie uwanja wa Taifa azunguke hata mara moja kama hataishia ICU. Na kama ni mzima, anatumia fedha za nchi kwenda kutibiwa nini ujerumani kila wakati au Ujerumani nako siku hizi kuna waganga wa kienyeji? 

Pili kwanini alikwenda kuombewa kwa Emmanuel Ministries huko Nigeria? Kampeni za Urais zinahitaji afya nzuri, sio mzaha kuweka mgonjwa akatufia kwenye jukwaa! Kuhusu tuhuma ya rushwa toka kwa Kimaro, nina hakika Kimaro bado yupo hai, na kama ni mkweli aseme ukweli. 

Kimaro ni rafiki yangu na nilimshawishi akawekeza hoteli ya Nyumbani sasa ni JB Belmonte, Mwanza. Sijachukua fedha ili nimpatie kitalu kwavile yeye sio mwindaji na sijasikia kuwa ana hiyo biashara. Ninachofahamu ana mahoteli na ndiyo biashara yake. Rais yupo kama alishaniita kunieleza hilo anaweza akasema, ni mkweli. 

Tuhuma za mimi kuhongwa na Kimaro alizianzisha Lowassa baada ya mimi kutaka kumuondoa Mkurugenzi wanyama pori wizara ya Maliasili. Mkurugenzi huyo alikuwa na mahusiano naye na baadae walikuja kuoza watoto wao. Hilo kila mtanzania analifahamu, na alimtetea sana abaki wizarani wakati huo. Lowassa yupo kwenye mtandao wa yote yanayosemwa kuhusu wanyama pori.

Pia tuhuma za kumtapeli aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Mhe Karume ndio nazisikia leo. Karume sijafika nyumbani kwake Zanzibar na wala hata alipokuwa Ikulu Zanzibar. Yupo na anaweza kuulizwa, ni mkweli atasema yaliyo kweli.

Huyo msichana anayesemekana nilimpa mimba, mhudumu wa Dodoma hotel, ndiyo namsikia leo, na kama yupo aniletee mtoto huyo kwani ndio nasikia kwenye watu wa Lowassa baada ya kuweweseka na machache tu tuliyoyaweka hadharani. 

Mwisho la kupewa fedha na mtuhumiwa wa IPTL nalo jipya simfahamu, labda Lowassa anamfahamu! Tatizo la huyu Lowassa, ni kupata URAIS, asipoupata sijui kama atabaki na afya ya kuridhisha. Anatuhumu watu tusiounga mkono jitihada zake tu, je wanaogombea watakuwa na hali gani mbele yake? Ushauri wa bure kwa wapambe wa Lowassa: Kuleni fedha yake maana ni halali yenu, fedha za kukwapua kwa njia zisizo halali ni haki ya kila mtu kuzitafuna, ila Urais hatopata. Kidumu CCM.



No comments: