Monday, February 25, 2008

Ana kwa ana na

Nazir Mustafa Karamagi



Charles Mullinda

JUMATANO, Februari 20, Tanzania Daima Jumapili ilifanya mahojiano na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Mustafa Karamagi, kuhusu mustakabali wake kisiasa baada ya kujiuzulu wadhifa wa uwaziri na jinsi alivyoipokea Ripoti ya Kamati Teule ya Bunge, iliyochunguza mchakato wa zabuni ya uzalishaji umeme wa dharura ulioipa ushindi Richmond Development Company LLC ya Huston, Texas, Marekani. Yafutayo ni mahoajino baina ya Mwandishi Wetu Charles Mullinda na Karamagi.

SWALI: Kisiasa, una mipango gani baada ya kujiuzulu wadhifa uliokuwa nao wa uwaziri?

JIBU: Nguvu kubwa sasa naielekeza jimboni kwangu, kuna mambo mengi yananisuburi huko. Nilipokuwa waziri nilikuwa na nafasi ndogo ya kuyashughulikia, majukumu yalikuwa mengi. Lakini kwa sasa ninayo nafasi ya kutosha ya kuwafanyia wapiga kura wangu kile nilichowaahidi katika kipindi hiki cha miaka miwili hivi iliyobakia.

Na hapa niseme hivi, najua ulitaka kusikia hilo, na wengi wanataka kusikia. Kwamba mimi katika uchaguzi wa mwaka 2005, sikugombea uwaziri, niligombea ubunge, niliposhinda ndipo Rais Jakaya Kikwete akaona ninaweza kumsaidia katika serikali, akaniteua.

Lakini wapo wengi tu katika chama chetu wanaoweza kuwa mawaziri. Mimi nimetoa mchango wangu mpaka nilipofikia, nimewaachia wenzangu nao waendelee, sina kinyongo kabisa, uwaziri ni mambo ya kupita tu, ulikuja kama ulivyoondoka.

SWALI: Uliipokeaje Ripoti ya Kamati Teule ya Bunge iliyokuwa chini ya uenyekiti wa Dk. Harrison Mwakyembe kuhusu Richmond na una maoni gani kuhusu ripoti hiyo?

JIBU: Katika baadhi ya maeneo niliipokea vizuri. Lakini katika maeneo mengine niliipokea vibaya, hasa maeneo yaliyolenga kutafuta watu. Walipotosha sana. Walipotosha hali halisi ilivyokuwa.

Nianze na jinsi nilivyoipokea kiujumla. Kamati ilikuwa inatafuta kitu kilichotokea, ilikuwa na mamlaka kisheria katika kutekeleza majukumu yake na ilijengewa uwezo wa kutopokea maneno ya umbea kwa sababu ilikuwa inawaapisha wahojiwa. Walikuwa wakitoa maelezo yao chini ya kiapo.

Sasa kamati iliposema kwamba imeumwa sikio, yaani mtu anatoa maelezo yake chini ya kiapo, hayo ndiyo yanayokubalika kisheria, baadaye mtu akiwa nje ya kiapo anaiuma sikio kamati, maneno ya umbea na kamati inayaweka katika ripoti yake, ni jambo la kushangaza na kusikitisha sana.

Kuruhusu umbea kuingia katika ripoti ya kamati kuliharibu maana nzima ya ripoti hiyo, ambayo katika baadhi ya maeneo ni nzuri. Walikuwa na uwezo wa kuwaita mashahidi mara ya pili kuwahoji, na wapo waliowaita mara ya pili.

Kwa hawa waliokuwa wakitoa maelezo ya kuuma sikio, ya umbea, kamati ilipaswa kuwaita mara ya pili na kuwaapisha kisha kuwataka watoe maelezo hayo chini ya kiapo ili uwe ushahidi rasmi. Hapo wangekuwa wamethibitisha habari hizo za kuumwa sikio.

Ingekuwa hivyo, ripoti nzima ingekuwa na nguvu kama walivyosema kwamba, walilazimika kuyachomeka maneno yale kulingana na uzito wa suala lenyewe.

Uliza mtu yeyote makini. Katika hili, atakwambia wanakamati walifurahia kuingiza umbea katika ripoti yao. Kwa sababu ni kama mtu anasimama mbele ya umati wa watu na kusema jamani tumeumwa sikio mtu fulani ni mwizi, lakini hatuna ushahidi. Hapo unakuwa umechafua jina la mtu huyo kwa tetesi, sasa ikidhihirika kuwa si mwizi, yule aliyekuuma sikio hakukwambia ukweli, unafanyaje wakati umeshamchafua mtu mbele ya jamii?

Hiyo ni kwa ujumla. Sasa kwa upande wangu binafsi, ripoti hiyo imenichafua kwa makusudi, jambo hili ni baya kabisa, lakini Watanzania wanapaswa kuelewa ukweli. Na siyasemi haya kwa sababu ninataka uwaziri, hapana kabisa, nimekwishatoka huko, nina kazi zangu, ninayasema kwa faida ya umma ili uelewe kuwa kulikuwa na mchezo mchafu uliopangwa makusudi na kundi la watu fulani kwa ajili ya kutuchafua.

Mimi nilihamishiwa Wizara ya Nishati na Madini, Oktoba 19, 2006. Hiyo ilikuwa ni siku sita baada ya Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO kuiandikia barua serikali kuhusu hali halisi ya tatizo la umeme nchini, udhaifu wa Richmond na walichokuwa wakipendekeza kifanyike.

Barua hiyo hii hapa (anaionyesha), waliandika Oktoba 13, 2006 wakieleza mambo mengi, baadhi ni kwamba baada ya wiki moja au mbili umeme ungekatika kabisa kutokana na maji kukauka katika mabwawa yanayozalisha umeme.

Iliichambua pia Kampuni ya Richmond jinsi walivyoshindwa kutekeleza mkataba wao. Utapeli wao, jinsi walivyokuwa wakidanganya kuhusu uletaji wa mitambo wakati kumbe ilikuwa haipo. Walishauri kuwa muda huo haukuwa wakati wa malumbano na Richmond, bali kukabiliana na tatizo lililokuwa likiikabili nchi.

Hivyo, mimi sikuhusika kabisa na mkataba wa Richmond, sikuwa katika wizara hiyo wakati unasainiwa, nilipoingia pale nilichokuta mezani ni ile barua ya Tanesco iliyokuwa imesainiwa na Mwenyekiti wa Bodi, Balozi Kazaura. Taifa lilikuwa katika tishio la kukumbwa na giza, nikawa katika shinikizo la kufanya kazi kufa na kupona hali hiyo isitokee, nikaanza kufanyia kazi mapendekezo ya barua ile.

Katika ushauri wao, walishauri kwamba, kwa sababu tayari Richmond ni tatizo, ilishathibitika kuwa haiwezi tena kuzalisha umeme katika kipindi kilichopangwa wakati taifa lilikuwa mbioni kukumbwa na giza. Walipendekeza kununuliwa kwa mashine za kuzalisha umeme wa megawati 40 kwa mikoa ya Kanda ya Ziwa iliyokuwa hatarini zaidi na wakaiomba serikali isaidie kutoa fungu la fedha kwa ajili ya kununulia mafuta ya kuendesha mitambo hiyo.

Pia walipendekeza kununuliwa kwa mashine ya kuzalisha umeme wa megawati 30 kwa Mkoa wa Dar es Salaam.

Mimi pamoja na wenzangu pale wizarani, tukaona walichoongea ni cha kweli, hivyo tukaanza kazi. Sasa hapo sijui nilishabikia vipi mimi Richmond kupewa zabuni ile!! Ninachoweza kusema kwa kauli yangu thabiti ni kwamba sikuhusika kushabikia Richmond wala kushinikiza ipewe kitu chochote, ushahidi ni barua hii (anaionyesha tena). Hapa nilisingiziwa kabisa na kamati ile, lengo lilikuwa kuchafua, na kweli wamenichafua!

Lakini ajabu zaidi, wakati kamati inasema mimi nilishinikiza TANESCO, walichotumia wao katika ripoti yao ni barua iliyoandikwa na Meneja wa Net Group Solution ambao tayari walikuwa mbioni kuondoka baada ya serikali kukataa kuwaongezea mkataba.

Hawa walikuwa wanaweza kuandika jambo lolote la ajabu kwa sababu ya kunyimwa kuongezewa mkataba kwa ajili tu ya kupotosha ukweli.

Lakini barua hii ya Tanesco ambayo mimi na wenzangu pale wizarani tuliifanyia kazi, hawakuitumia kabisa katika ripoti yao. Barua ambayo nilimtumia Spika Samuel Sitta, inaeleza jinsi wizara ilivyokuwa ikifanyia kazi mapendekezo ya Tanesco.

Na hata wakati Richmond ilipoandika kuomba kukabidhi shughuli zake kwa Dowans. Kweli nilikuwa nje, lakini nilipopata tu habari hizo nilimpigia simu Mwenyekiti wa Bodi, Balozi Kazaura, nikamtaka ajiridhishe kwanza na Richmond yenyewe na kama mkataba unaruhusu jambo kama hilo.

Katika ripoti yao wameeleza hivyo. Sasa kama kweli nilishabikia ningetoa maelekezo hayo? Nasisitiza, ni ripoti yenye baadhi ya mambo ya kuumba kwa ajili ya kutuchafua.

SWALI: Kwa wadhifa uliokuwa nao, ulikuwa ukiwasiliana na rais. Je, mliwahi kumwambia ukweli kuhusu Richmond?

JIBU: Alikuwa na taarifa, lakini kuna wasaidizi wake, sisi tuliokuwa tukishughulikia jambo hili, hivyo aliamini kabisa kuwa tutapigana kufa na kupona kuinusuru nchi na tatizo hilo na ndivyo tulivyofanya.

Suala la utapeli wa Richmond serikali ililijua, tulijua kuwa ni matapeli ndio maana tukawa tunawatilia shaka katika kila hatua waliyokuwa wakijaribu kufanya wakati mimi nikiwa pale wizarani. Tungeweza kuvunja mkataba nao, lakini wanasheria walishauri kuwa watatusumbua, tutaanza kupelekana mahakamani na wanaweza kuzuia kufanyika jitihada nyingine za kupata umeme, kwa sababu tulikuwa na mkataba nao.

Hapo tukaamua kuwaacha kwanza huku tukiwa tumezuia malipo yao, tukaanza jitihada za kupata njia mbadala ya kupata umeme. Nashukuru Mungu wakati kazi hiyo ikiendelea mvua zilianza kunyesha, hali ikabadilika.

Hata kuunda kamati teule, mimi naamini kuwa rais aliamini itafanya kazi ya kweli na kutoa ripoti ya kweli. Rais anaziamini taasisi zilizopo zinazoongoza dola, yaani bunge, mahakama na serikali. Huo ndio msingi wa rais kuiachia kamati ifanye kazi kwa uhuru.

Kinyume chake, watendaji katika taasisi hizi tunatumia nafasi ya kuaminiwa na kiongozi mkuu wa nchi kuchafuana, kumalizana kisiasa. Na kama alivyosema rais, wakati akimzungumzia Lowassa kuwa historia itamuhukumu. Ni kweli kwa sababu kilichozungumzwa na kamati ni tofauti kabisa na ukweli halisi, hivyo ipo siku ukweli utakuwa bayana na historia itahukumu.

SWALI: Kwa maneno yako, una maana wanaCCM mnachafuana, una mawazo gani kuhusu kuendelea kuwa mwanaCCM kulingana na hali ilivyo?

JIBU: Chama ni taasisi, si kundi la watu au mtu, au vitendo vyao. Mtu au kundi la watu hawawezi kuniondoa CCM kwa vitendo vyao visivyokubalika, ili mradi nimeshajua chimbuko la watu hao. Ningeweza kufikiria kuachana na chama kama kingebadili katiba yake.

Sina tatizo na CCM. Nina matatizo na baadhi ya watu ambao wameamua kunichafua mimi na baadhi ya wanaCCM wenzangu. Watu ambao kwa makusudi wameamua kutosema ukweli kwa malengo yao.

Hawa wataleta matatizo ndani ya chama na serikali. Lakini mimi bado ni mwanaCCM, ni mbunge, nitapambana na waliokusudia kunimaliza kisiasa, kuna vikao ndani ya chama ambako nimepanga kwenda kusema kila kitu. Sitaacha kufanya kazi zangu za kisiasa, sitawaangusha wapiga kura wangu, wasiwe na hofu. Na mwaka 2010 nikiona mchango wangu bado unahitajika kwa wapiga kura wangu, kama bado watakuwa wananihitaji, nitagombea tena.

SWALI: Unatajwa kuwa mmiliki wa Kampuni ya TICTS inayoshughulika na upakiaji na upakuaji wa makontena bandarini. Kampuni hii inadaiwa kuongezewa mkataba wa miaka 15 kinyume cha taratibu kwa msaada wa Rais mstaafu Benjamin Mkapa. Unalizungumziaje hili?

JIBU: Kweli ninahusika katika TICTS, sio siri, na ni kweli iliongezewa mkataba wa miaka 15. Lakini si kinyemela, taratibu zote zilifuatwa, ndiyo maana sina wasiwasi. Kila kitu kipo.

Nieleze kirefu hapa ili twende pamoja. Kwanza wakati TICTS inaomba kuongezewa mkataba, sikuwa na uhusiano wowote na Mkapa. Naomba ieleweke hivyo, kwamba hakushiriki kwa namna yoyote kuweka mkono wake katika hili. Sisi wenyewe tuliomba kwa sababu zilizo wazi kabisa za kibiashara.

Mwaka 2000, TICTS iliingia mkataba na serikali kupitia Tume ya Kurekebisha Mashirika ya Umma (PSRC) wa kupakua na kupakia makontena katika bandari ya Dar es Salaam.

Wakati huo, kwa mwaka bandari ya Dar es Salaam ilikuwa inapokea wastani wa kontena 100,000, lakini uwezo wake ulikuwa kupokea kontena 250,000 kwa mwaka.

Tuliingia mkataba huo baada ya wataalamu wa bandari kufanya tathmini na kuona kuwa kama atapatikana mwekezaji wa kufanya kazi hiyo katika muda wa kipindi cha miaka 10, kulingana na hali ya vifaa ilivyokuwa bandarini, hatahitaji kuwekeza mtaji mkubwa sana, mtaji wake usingezidi dola za Marekani milioni 2.5.

Tulifanya kazi hiyo kuanzia mwaka 2000 hadi 2004, idadi ya upakuaji kontena ikawa imeongezeka kutoka 100,000 hadi 214,000 kwa mwaka, lilikuwa ni ongezeko kubwa.

Tukaiandikia serikali kuieleza jinsi kontena zilivyoongezeka na kwamba uwezo wa bandari wa kupakua kontena 250,000 kwa mwaka ulikuwa unakaribia kupitwa.

Tuliieleza serikali kuwa kwa sababu bandari ya Dar es Salaam ilikuwa ya kwanza Afrika, kama tunataka iendelee kuwa ya kwanza, basi kulikuwa na kila sababu ya kuanza kufikiria mpango wa kupanua bandari hiyo na pia kuweka mashine za kupakua kontena kulingana na mzigo uliokuwa ukiingia.

Tulieleza wazi kuwa uwekezaji uliokuwa ukihitajika bandarini hapo ni mkubwa, hivyo kulihitajika eneo kubwa zaidi na muda zaidi ili uendane na gharama za uwekezaji unaohitajika.

Ilipofika Aprili 2005, tayari kiwango cha uingiaji kontena kilishazidi, kilishafikia kontena 270,000 na serikali ilikuwa bado kimya. Kelele zilianza baada ya msongamano kuwa mkubwa, lakini serikali bado haikutoa maamuzi.

Serikali ilitoa maamuzi Agosti 2005, ikaitaka PSRC ianze majadiliano na TICTS ya jinsi ya kuongeza mkataba kulingana na mahitaji ya uwekezaji yalivyokuwa. Hivyo ndivyo ilivyokuwa, majadiliano yalifanyika mkataba ukaongezwa sasa tunafanyia kazi yale tuliyokubaliana.

Sasa wanaosema mkataba ukatishwe hawajui wanasema nini, lakini mimi naamini serikali iko makini kwa sababu kila kitu kiko bayana. Na kila siku idadi ya kontena zinazoingia inazidi kuongezeka, sasa zinafikia 350,000 kwa mwaka na tunategemea zitaongezeka zaidi hadi 400,000 hivi karibuni.

SWALI: Kuna taarifa kwamba umeamua kuingia katika biashara ya vyombo vya habari kwa lengo la kupambana na mahasimu wako kisiasa, unazizungumziaje taarifa hizi?

JIBU: Mimi ni mfanyabiashara, nikiona biashara nzuri siwezi kuacha kuifanya.


Kutoka Tanzania Daima





No comments: