Monday, February 01, 2010

Ushauri kwa Jerry Muro toka kwa Da´Subi



Tangu kuripotiwa kwa taarifa kuwa mwandishi Jerry Muro (pichani) amekamatwa kwa muda na kuwekwa chini ya ulinzi kwa 'tuhuma' za kupokea rushwa ya shilingi za Kitanzania milioni kumi, kisha taarifa kubadilishwa kuwa anatuhimiwa kwa kukutwa na pingu (nyara za Serikali), na baada ya kumsikia mwenyewe akizungumza, nimetafakari na kujiweka katika nafasiyake kwa sas na kujiona nipo katika hali ya wasiwasi, woga na kukosa imani na hata usalama wa uhai wangu kuwa hatarini.

Nafahamu fikakuwa ni mapema kuzungumza kuhusu suala hili, lakini wakati mwingine mambo huhitaji uharaka kuliko kusubiri hadi yakaharibika kabisa. Inabidi kulizungumzia ili kutoa ushauri kwa marafiki wa kweli wa karibu, ndugu na jamaa wa Jerry katika kufikisha mawazo binafsi.

Jerry anahitaji kupata mapumziko. Kikazi, anahitaji kutuliza akili ili aweze kuwa na ufanisi. Kimwili, anahitaji kutulia ili kupevusha fikra ili kujiepusha na mkanganyiko wa mawazo (frustration) unaoweza kusababishwa na kuwaza mambo mengi na mazito kwa mkupuo.

Jerry anahitaji marafiki jasiri na walio tayari kupambana wakati wowote, hasa kwa wakati huu kuliko wakati mwingine wowote. Amekuwa na maadui wengi kuliko marafiki kutokana na kazi yake.

Jerry anahitaji washauri wachache makini. Washauri wanapokuwa wengi, ni vigumu kutilia maanani na kufuata ushauri unaotolewa, hivyo watu wachache wenye ufahamu au katika fani ya ushauri wanaweza kumwelewesha umuhimu wa kutulia, kupumzika na kujipanga upya.

Jerry anahitaji kuwa mkimya kwa sasa. Si vyema kwake kuendelea kuongelea suala hili hasa baada ya kuwa limeshafikishwa katika vyombo vya sheria ili kuchukua mkondo wake. Ni kweli kuwa mambo ya kusingizia yanaudhi na hayavumiliki lakini vile vile upande wa mashtaka unaweza kuwa na sababu ya kuuthibitishia umma au kuufanya umma uamini kuwa Jerry alitenda uhalifu. Mambo haya yanahitaji wahusika wa kitaalamu zaidi, ni vyema Jerry akawapata wataalam wa nje na ndani kwa ajili ya kupambana na suala hili.

Jerry anahitaji kusafiri, si tu nje ya mkoa wa Dar Es Salaam, bali nje kabisa ya nchi. (Hii itategemea kama ana ruhusa ya kufanya hivyo kutokana na yanayomsibu). Anahitaji kupata muda wa kutosha wa kumwezesha kufikiri vyema namna ya kukabiliana na tuhuma zinazomhusu kwa mujibu wa sheria na haki. 

Sipo tayari kusema kuwa Jerry apunguze kasi ya mapambano aliyoianza, nadhani kama amejitoa muhanga kwa kazi hii ili kuendeleza mapambabo, basi atakuwa tayari kwa lolote ila kama ilivyo vita nyingine yoyote, lazima upange mashambulizi kwa makini ukiwasoma wapinzani wako mbinu zao na jinsi ya kuzishinda. Ndiyo maana bado ninasisitiza kuwa, Jerry anahitaji mapumziko. Kwa muda mfupi ameonyesha ukomavu na kutoa mwanga katika uandishi tafiti (investigavite journalism), ila nipo tayari kusema kuwa Jerry anahitaji kufahamu kuwa maji aliyoyavulia nguo kuyaoga ni ya kina kirefu, yenye mawimbi makali ndani ya ziwa pana sana. Ndani ya ziwa hilo wapo wanaofurahi kuogelea na Jerry lakini katika hao pia wamo wanaomvizia ili kumsokomeza kichwa katika maji marefu ili azame, akose pumzi na ikibidi afilie mbali. Jerry ameonesha mfano mzuri sana kwa kufichua maovu kwani ndicho tunahochitaji sana nchini Tanzania ili kuweza kumulika wala rushwa, wabadhirifu wa mali ya umma na wakandamizaji wa raia.

Huu nimtizamo binafsi na ambao ningeutumia au ningemshauri mtu yeyote aliyekumbwa na hali kama hii.

Nimeandika haya kufuatia video niliyoiona hivi punde kuhusu Jerry alivyozungumzia kadhia aliyokumbana nayo akiwa mikononi mwa polisi.

No comments: