JINAMIZI la kashfa za ufisadi limeendelea
kuwaandama Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa na aliyekuwa
Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye sasa ni Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew
Chenge (CCM), kuwa ndio waliouza nchi katika utawala wao.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa
Ibrahim Lipumba, ndiye aliyewataja viongozi hao kuuza nchi kwa wageni
wanaochimba madini yanayowanufaisha zaidi wageni kuliko Watanzania.
Profesa Lipumba alitoa kauli hiyo jana jijini
Mwanza alipokuwa akijibu swali la mwandishi wa Tanzania Daima Jumapili, muda
mfupi baada ya kuahirishwa kwa muda mkutano wa kujadili na kuchangia mawazo juu
ya maendeleo kwa wote katika Mkoa wa Mwanza.
“Kizazi hiki na kijacho viwatupie lawama Mkapa na
Chenge, hawa wameliingiza taifa kwenye mikataba ya unyonyaji ya sekta ya madini
inayowaneemesha zaidi Wazungu wanaojua thamani na umuhimu wa dhababu kuliko
Watanzania wenye ardhi inayotoa madini husika,” alisema.
Alibainisha kuwa Tanzania inatafunwa na saratani
mbaya ya mikataba mibovu ya madini iliyoasisiwa na Mkapa kwa kushirikiana na
Chenge katika utawala wa Awamu ya Tatu iliyosifika kwa sera ya ubinafsishaji wa
mali za umma zilizokabidhiwa kwa wawekezaji wengi wao kutoka nje ya nchi.
No comments:
Post a Comment