Thursday, March 27, 2014

Haki ya Watanzania kuzaliwa ughaibuni



Taifa letu likiwa katika mpito na wakati mgumu wa kuandika rasimu ya katiba mpya ya watanzania, hatuna budi kuweka kando itikadi zetu za kisiasa, tofauti za kiimani na hata maslahi binafsi ili tuungane katika kutafuta katiba itakayokidhi mahitaji yetu ya sasa na ya vizazi vijavyo. 

Katika mchakato huu, inatubidi tuwe makini na wakweli katika kujadili hatma na haki ya kuzaliwa ya ndugu zetu ambao wanaishi ughaibuni. Lazima tuwajumuishe na kuwapa haki zao za msingi; haki ya kuzaliwa katika ardhi ya Tanzania ambayo ni zawadi kutoka kwa mwenyezi Mungu. Hii ni haki ambayo kamwe haiwezi kubatilishwa na mamlaka ya aina yeyote wala haiwezi kutenguliwa na binadamu yoyote. Ni kujidanganya kudai kwamba waliochukua uraia wa kigeni warudi Tanzania kama wageni. 

Kwa makusudi kabisa, nimeamua kuchokonoa huu mjadala wa haki ya kuzaliwa nikiwa na sababu nyingi za manufaa kwa taifa letu; ya msingi ikiwa ni sababu ya kiuchumi na hatma ya taifa letu. Jamii ya watanzania wanaoishi ughaibuni ni hazina adimu ya rasilimali watu wanaohitajika katika maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii ya Tanzania. 

Ni kundi lenye uwezo mkubwa wa kiuchumi ambao lazima tuwakumbatie. Mheshimiwa Rais Jakaya kikwete, Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Waheshimiwa Dr. Wilibrod Slaa, Freeman Mbowe, Bernard Membe, wote, kwa kipindi kirefu wameunga mkono haki ya kuzaliwa ya watanzania wanaoishi ughaibuni kupata haki zao za msingi za kurudi katika ardhi yao ya kuzaliwa bila masharti wala vikwazo vya aina yoyote

Bila shaka wapo wanasiasa wenye ajenda zao binafsi ambao wamekuwa kikwazo kikubwa katika kuwazuia wazawa wa Tanzania wanaoishi ughaibuni kupata haki sawa katika katiba mpya. Siwezi kuwalaumu, kwani pengine wengi hawana uelewa wa faida ambazo zitapatikana kwa kuwapa ndugu zetu waliozaliwa Tanzania haki ya kushiriki katika ujenzi wa taifa. 

Mjadala huu tuaouanzisha lazima uweke katika mizani faida na athari za kuwapa watanzania haki yao ya kuzaliwa na hatimaye kupata uwiano ambao utakidhi na kujibu maswali mazito ambayo ndio chanzo cha vikwazo vilivyopo kwa sasa.

Wiki chache zilizopita, Blogger-mwanasiasa mmoja nchini Tanzania alitoa shutuma dhidi ya watanzania wajulikanao kama wana Diasapora wanaodai haki zao za kuzaliwa katika ardhi ya Tanzania, huku akisahau kwamba yeye mwenyewe alikuwa mwana Diaspora kwa miaka takribani thelathini. Hata kama alikuwa na uraia wa nchi thelathini, mwisho wa siku alirudi katika ardhi aliyozaliwa yaani, Tanzania. Nina imani kwamba anao wanafamilia ughaibuni ambao ndoto yao kubwa ni kutambulika kama watanzania wenye haki zote ambazo kila mzawa anazo. 

Katika tafsiri isiyo rasmi ni kwamba amewatosa ndugu zake. Warudi Tanzania wasirudi siyo tatizo kwake. Tofauti na mategemeo ya wengi, huyu blogger alitegemewa kuwa mstari wa mbele kuhamasisha na kutetea haki za kuzaliwa za watanzania wanaoishi ughaibuni. 

Huyu blogger ndio picha kamili ya wanasiasa ambao mara nyingi hutafuta nafasi za kupiga picha na wanadiaspora pindi wanapotembea nchi nyingine ambako kuna watanzania. Wanasiasa hawahawa watakuwa mstari wa mbele kujipanga uwanja wa ndege kuonyesha huzuni na huruma na hata kumwaga machozi ya kinafiki pale majeneza ya wana Diaspora yanaporudishwa katika ardhi yao ya kuzaliwa huku wakiwanyima haki zao za kuzaliwa wanapokuwa hai. 

Wengi wa watanzania waliomba uraia wa nchi nyingine siyo kwamba hawalipendi taifa lao,la hasha! Wengi ni wazalendo waliolazimika kuchukua uraia wa nchi nyingine ili kupata ahueni kutokana na ugumu wa maisha unaowakabili mamilioni ya watanzania. Wengine walitafuta vibali vya kuishi ili wapate elimu ambayo Tanzania isingeweza kuwalipia. 

Badala ya kutafuta chimbuko la tatizo au wazo fulani, ni desturi yetu kama jamii kwa mjumbe kusulubiwa na hata kuuwawa ili kuliua wazo au jambo linalotishia maslahi ya wachache. Kumshambulia John Mashaka mathalani, hakutaweza kamwe kuliua swala ambalo wakati wake umewadia. Binafsi nimeamua kubaki na uraia wangu wa kitanzania licha ya kuwa na nafasi ya kuchukua uraia wa nchi nyingine. Kubwa ya yote, ninajikita kuanzisha huu mjadala ili kuitetea Tanzania na rasilimali zake hasa rasilimali watu. 

Kama taifa, tunawahitaji ndugu zetu wenye taaluma mbali mbali waliotapakaa kote duniani na hata kufikia hatua ya kuchukua uraia wa nchi nyingine. Napigania watanzania milioni 45 nikizingatia faida za kiuchumi, kisiasa, kijamii ambazo zinapatikana na rasilimali watu wenye asili ya kitanzania. Wazawa wanaopigania haki zao za kuzaliwa pamoja na vizazi vyao.

Ni muhimu hawa wanasiasa wakakumbushwa kuhusiana na maamuzi yao ya kuwatenga watanzania walio nje ya nchi, hususan kuwanyima haki zao za kuzaliwa. Inabidi wakumbushwe kwamba, wazaliwa wa Tanzania wanaoishi ughaibuni wana ndugu zao Tanzania, ambao ndio wapiga kura wao. Na ikiwa wanaamua kwa makusudi kuwatenga, basi kundi hili maarufu kama Diaspora watumie uwezo wao, ushawishi wao na mbinu zote walizo nazo kuwaadhibu wanasiasa wanaozuia haki zao za kuzaliwa

Pengine niwakumbushie viongozi wa jumuiya za watanzania popote walipo duniani kwamba haki haiombwi. Haki inadaiwa, na asiyeweza kudai haki yake na hata kuiona haki yake kama zawadi au upendeleo fulani basi huyo amepoteza haki yake ya kuishi. 

Viongozi wa jumuiya za watanzania ughaibuni hawana budi kuonyesha uwezo wao wa kuongoza kwa kuwa mstari wa mbele wakiwahamasisha watanzania waliotapakaa duniani kudai haki zao za kuzaliwa. Inabidi wapaze sauti zaidi ili viongozi wetu walioweka pamba masikioni wasikie madai yao. Mashabiki wa CCM ,CUF, CHADEMA na wengineo wote wataathirika sawa. Kwa maana hiyo, vita hivi havina mipaka, ni vita vya watanzania wa matabaka yote. Wana diaspora lazima wawe na mshikamano kama watanzania.

Mungu Ibariki Tanzania
John Mashaka
mashaka.john@yahoo.com

No comments: