Sunday, April 20, 2014

MCHAKATO WA KATIBA MPYA - UJUMBE WA KICHUNGAJI WA PASAKA 2014 KWA WAAMINI NA WATU WOTE WENYE MAPENZI MEMA




“Sote tuwe na Umoja” (rej. Yn 17:21)

UTANGULIZI:

Ndugu wapendwa, tunapohitimisha kipindi cha Kwaresima kilichokuwa na ujumbe: “Ukweli utawaweka huru” (Yn. 8: 32), tunawaletea ujumbe wa “Umoja” ili kuongeza msisitizo kwenye ujumbe wetu wa Kwaresma. Tunaitwa kukubali kuwa umoja ni ukweli msingi wa kila mafanikio ya jumuiya ya mwanadamu.

Ufufuko ni Pasaka inayomaanisha kivuko au kupita kwa Wayahudi toka kwenye matatizo ya utumwa hadi uhuru kamili. Kwa Wakristo ni kuvuka kutoka utumwa wa fikra za kifo (dhambi) hadi uhuru kamili wa ufufuko wetu na Bwana Yesu. Kwahiyo, furaha za Pasaka zinapaswa kusheheni shukurani za dhati kwa zawadi nyingi alizotujalia Mungu Muumba wetu tokea mwanzo na hasa nyakati hizi katika mwanga wa Ufufuko wa Kristo.

Adhimisho la Pasaka litawaliwe na furaha, amani na matumaini makuu yaliyoletwa kwa Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. Mtume Paulo anatuambia: “Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo” (1Kor. 15:57).

Wakati dhambi na kifo husababisha kujitenga; uhuru, furaha na amani husababisha kuungana. Ndivyo ilivyotokea kwa Adamu na Eva. Walipokuwa bila dhambi walikuwa huru, wenye furaha, amani na umoja na Mungu. Walipotenda dhambi walimkimbia Mungu, wakatafuta kujificha. Hata wao wenyewe walioneana aibu na hatimaye wakafukuzwa kutoka kwenye bustani ya Edeni (Mwa. 2:25; 3:7-8, 23-24).

1.Ndugu zetu katika Kristo, “Amani iwe Kwenu” (Yn. 20:19). Wakati huu wa Pasaka, wakati ambao pia mchakato wa kuandika Katiba ya nchi yetu unaendelea, hatuwezi kuacha kutafakari kwa dhati juu ya umoja wetu sisi Watanzania. Bila shaka, moja ya mihimili mikubwa ya umoja wa kitaifa ni uongozi bora.

Mwenyezi Mungu aliwatoa watu wake utumwani Misri na kuwaweka huru kwa kuwateulia viongozi miongoni mwao. Kiongozi wa kwanza alikuwa Musa (Kut. 3:10).

• Chini ya uongozi wa Musa Wayahudi walichukua muda mrefu kujenga umoja na uelewa, kwamba walikuwa watu wa Mungu na walipaswa kumtambua kiongozi wao kama mteule wa Mungu (Kut. 16:3; 17:4;).

• Katika kutangatanga kwao jangwani, iliwachukua pia muda mrefu kutambua uovu wao na kujitakasa dhidi ya dhambi zao (Kut. 32:1-14).

• Hata wakiwa tayari katika nchi waliyoahidiwa hawakuacha machukizo yao kwa Mungu pamoja na kukanywa mara kwa mara na Manabii wake Mwenyezi Mungu (Amu. 2:11-13).

Wakati ulipowadia, Mungu alimtuma Mwanae Yesu Kristo kujenga Utawala wa Mungu juu ya msingi wa imani na ukweli (Gal. 4:4):

• Imani kwa Mungu na imani baina ya watu wenyewe – kuaminiana – ndio msingi wa Utawala wa Mungu (2Thes. 2:13-17).

• Lakini kutokana na udhaifu wa kibinadamu, mara nyingi tunavunja umoja wetu na Mungu na kati yetu wenyewe kwa kiwango cha kutotaka kuishi pamoja; tunabaguana na hatutendeani haki (Mwa. 4:7-8).

Katika ulimwengu wa leo, tunashuhudia madhara ya utengano wa namna nyingi. Dhambi nyingi za binadamu zinasababisha mifarakano na vita. Hayo ni matukio ya kila mara katika nchi nyingi ulimwenguni na hasa kwetu Afrika. Hata historia yetu wenyewe ina matukio mengi ya jamii kufarakana na kujizamisha katika vita.

• Mababu zetu walipitia maisha marefu ya kuhamahama na kuchukuliwa utumwani na wengine kubaki watwana na watawaliwa wa kikoloni kwa vipindi virefu kabla ya kujipatia uhuru wa kujitawala.

• Tulipopata uhuru, tulijifunza kujenga umoja katika tofauti zetu kubwa za kikabila na kufikia taifa moja.

• Tulichukua hatua kubwa kuunganisha nchi mbili huru, Tanganyika na Zanzibar, na kuifanya kuwa nchi moja ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa kielelezo kwa Bara la Afrika cha kujenga umoja.

2.Hatua zote hizo tulizopitia na tulizochukua kwa makusudi kabisa, tulikuwa na nia na utashi wa kuwa wamoja. Tulitaka kujenga maendeleo ya pamoja na mafanikio ya kila Mtanzania kufikia maisha bora. Jitihada hizi njema zimekuwepo kwa miaka hamsini iliyopita. Tumefanikisha mambo mengi katika umoja wetu ambao unatusukuma kumshukuru Mungu. Kwa muda mrefu umoja wa Watanzania umeonekana kwa mataifa mengine kuwa ni kielelezo cha umoja wa kitaifa wa hali ya juu sana. Ni umoja uliokua kufikia kiasi cha kufuta tofauti za awali za mataifa yaliyohusika kuunda umoja.

Tunamshukru mwenyezi Mungu kwa kuifanya Nchi yetu kuwa kimbilio la waliokata tamaa. Tanzania imewapa wakimbizi mahali salama pa kuishi pamoja na Watanzania. Chini ya Jamhuhuri ya Muungano wa Tanzania, waliokuwa bado chini ya wakoloni, waliandaliwa kujikomboa na kuwa mataifa huru.

Pamoja na mafanikio hayo makubwa, zimejitokeza dosari kadhaa katika umoja zilizofanya umoja wetu upoteze baadhi ya sifa zake za awali. Kupungua kwa hisia za kujisikia watu wote ni taifa moja, ni dosari iliyoanza kukua taratibu na sasa inaonekana kuwa ndio ukweli. Baadhi ya Watanzania wanafikiri kuwa umoja unaofuta tofauti haufai ila umoja unaosisitiza tofauti kama ulivyo umoja wa kikanda (kama ilivyo SADC, ECOWAS, n.k) ndio unafaa! Wakati mataifa mengine yanatamani umoja unaofanana na ule umoja wetu wa awali, baadhi yetu tunatamani kurudi nyuma kwenye umoja wa mpito!

Kutokana na mapungufu yaliyodhihirika ndani ya mafanikio yetu, umuhimu wa kufanya marekebisho ulidhihirika. Ni kwa sababu hiyo, watu wengi walitaka na wanataka mabadiliko au mageuzi ya msingi sana. Kwa msukumo huo ndio sababu tuliingia katika mchakato wa kuandika Katiba Mpya.

3.Kazi ya kuandika Katiba si nyepesi na yataka umakini mkubwa. Haishangazi sana tunapojionea mivutano na migongano ya hoja kutoka kwa makundi kinzani katika nchi moja. Mawazo ya wengi yamewasilishwa kisheria na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa ajili ya kujadaliwa na Bunge Maalum la Katiba (BMK). Sasa, tunashuhudia makundi yenye nguvu yakijaribu kushinikiza kuingizwa matakwa yake kwenye Katiba kwa njia zozote zile ili kujihakikishia kuendelea kulinda maslahi yake ya kisiasa. Wajumbe wa Bunge Maalum Katiba wanazozana, wanakashifiana, wanatukanana na hawataki kuachana na itikadi za kisiasa ili kufikia muafaka katika masuala muhimu yatakayowahakikishia raia wa kawaida kushiriki kwenye fursa za maendeleo kwa manufaa ya wote. Hayo lakini yasitukatishe tamaa na kujiona kama tu watu wa kushindwa wakati tukiwa bado kwenye mchakato mrefu wa kujipatia jukwaa jipya kwa mustakabali wa taifa letu Tanzania.

Tushirikiane na wote wenye nia njema kupambana na nguvu za maovu na ubinafsi na kuachana na itikadi za kisiasa na matakwa ya kiuchumi ya matabaka ya walio nacho ili kupigania haki za wanyonge. Tuandae Katiba ambayo itatupatia misingi imara ya maadili itakayotuongoza kupigana dhidi ya ubinafsi na ufisadi, na kutetea haki za binadamu kwa wote. Vigezo vyote muhimu kwa maisha ya mshikamano kitaifa vimeandikwa katika Rasimu ya Katiba Sura ya 1 hadi ya 5. Tukisha kukubaliana na yaliyomo katika sura hizo, muundo wowote wa Serikali unawezekana kwa kuzingatia kanuni za uwiano wa madaraka na wajibu wa mihimili mitatu ya Dola kwa mujibu wa Sura za 8 hadi 15.

Ili tufikie lengo letu la kuwa na Katiba bora katika hatua tuliyofikia ya mchakato wa Katiba Mpya yatubidi kuzingatia yafuatayo:

• Kuheshimu kazi ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kuitumia kama ilivyokusudiwa na sheria iliyoiweka.

• Kuwa na nia njema ya kweli ya kutafuta suluhisho la matatizo mengi ya utendaji katika Dola zilizopo katika Muungano.

• Kuwa na hamu ya kujitoa kwa taifa na kulitumikia kwa moyo bila kutawaliwa na ubinafsi au kujipendelea kiinchi na kiukanda kwa madhumuni ya kuboresha maisha ya Watanzania wote.

• Chaguo la muundo wa Dola, sharti liongozwe na malengo na madhumuni ya umoja wetu wa kutaka tuishi kwa mshikamano wa dhati. Uchaguzi wa muuungano wa serikali moja, mbili au tatu sharti ufanywe kwa dhamiri safi iliyo na uelewa uliochambua matatizo yaliyopo ya Muungano na kuridhia mfumo utakaosuluhisha matatizo hayo pasipo mashaka yoyote.

4.Baada ya kutafakari historia ya ukombozi wa mwanadamu kwa ufupi na hatua Watanzania tuliyofikia katika uhuru wetu wakati huu wa adhimisho la Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo mwaka 2014, tungependa kwa namna ya pekee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumvuvia Rais Jakaya M. Kikwete ujasiri wa kuamua kuanzisha mchakato wa kuandika Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kisheria katika wakati muafaka.

Kwa mchakato huo wa Katiba, kupitia Tume yake Huru, Watanzania wamepata fursa ya kusema kila jambo lililowaelemea maishani na kuainisha namna wanavyotaka kujitawala. Wakati ulikuwa mwafaka kwa sababu kulikuwa na manung’uniko mengi ya ukiukwaji wa Katiba ya sasa ambayo hayakuweza kujibiwa na Serikali zilizopo. Hatua ya kuamua kuyakabili hayo kwa sheria ya Kurekebisha Katiba iliwapa wananchi fursa ya kutoa maoni yao bila mizozo na machafuko.

5.Tume ya Mabadiliko ya Katiba imewasilisha kwenye Bunge Maalum la Katiba Rasimu ya Katiba iliyotokana na maoni huru ya watu binafsi na makundi mbali mbali zikiwemo taasisi za dini, mamlaka za kiserikali na asasi huru za kiraia. Tunalisihi na kulishauri Bunge Maalum la Katiba kuheshimu mawazo yaliyowasilishwa na kutumia busara zilizopendekezwa za kujenga muundo wa Muungano utakaokidhi mahitaji ya utangamano, mshikamano, amani, maadili, uhuru na uwajibikaji wa viongozi na raia wa Tanzania.

HITIMISHO

Ndugu wapendwa,

Wakati huu wa Pasaka, tuendelee kuliombea Bunge Maalumu la Katiba ili wajumbe wawe wazingatifu wa matakwa na matarajio ya Watanzania yalivyoainishwa katika Rasimu ya Pili ya Katiba na Tume ya mabadiliko ya Katiba kwa kuheshimu maoni ya Watanzania na kuboresha maoni hayo kwa hekima na busara ili kulinda mstakabali wa Taifa letu; Tanzania yenye amani kwa ustawi wa watu wote.

“Ingekuwa heri leo msikie sauti hii; msifanye migumu mioyo yenu”. (rej. Zab 95:7-8)

Tuombe:

Ee Bwana, katika upendo wako uwape neema watu wa taifa lako, waishio Tanzania. Katika upendo wako ujenge tena nguzo za imani, matumaini na mapendo katika mji nchi yetu. Watanzania wakiwa na imani, matumaini na mapendo ya haki utapendezwa na sadaka wakutoleazo; kila mtu akijitolea yeye mwenyewe kwako kama sadaka safi juu ya altare, pamoja na katika Kristo Mfufuka aliye katika Ekaristi.

Mama Bikira Maria atuombee ili ndani yetu uzaliwe upya uaminifu unaotupa uwezo wa kutangaza kazi kuu ya Mungu. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.


Amani ya Kristo Mfufuka iwe nanyi


Ni sisi Maaskofu wenu:

1. Mhashamu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Askofu wa Iringa
2. Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Dar es Salaam
3. Mhashamu Askofu Mkuu Josaphat Lebulu, Arusha
4. Mhashamu Askofu Mkuu Paul Ruzoka, Tabora/Kigoma Msimamizi
5. Mhashamu Askofu Telesphor Mkude, Morogoro
6. Mhashamu Askofu Gabriel Mmole, Mtwara
7. Mhashamu Askofu Mkuu Yuda Thaddaeus Ruwa’ichi, Ofm Cap, Mwanza,/Shinyanga
8. Mhashamu Askofu Bruno Ngonyani, Lindi
9. Mhashamu Askofu Anthony Banzi, Tanga
10. Mhashamu Askofu Agapiti Ndorobo, Mahenge
11. Mhashamu Askofu Evaristo Chengula, IMC, Mbeya
12. Mhashamu Askofu Augustino Shao, Cssp, Zanzibar
13. Mhashamu Askofu Damian Kyaruzi, Sumbawanga
14. Mhashamu Askofu Severine NiweMugizi, Rulenge-Ngara
15. Mhashamu Askofu Desiderius Rwoma, Bukoba /Singida Msimamizi
16. Mhashamu Askofu Method Kilaini, Bukoba
17. Mhashamu Askofu Damian Dallu, Geita/Askofu Mkuu Mteule Songea
18. Mhashamu Askofu Ludovick Minde, OSS, Kahama
19. Mhashamu Askofu Alfred Leonard Maluma, Njombe
20. Mhashamu Askofu Castor Paul Msemwa, Tunduru-Masasi
21. Mhashamu Askofu Beatus Kinyaiya, Ofm Cap, Mbulu
22. Mhashamu Askofu Michael Msonganzila, Musoma
23. Mhashamu Askofu Issac Amani, Moshi
24. Mhashamu Askofu Almachius Rweyongeza, Kayanga
25. Mhashamu Askofu Rogath Kimaryo, Same
26. Mhashamu Askofu Salutaris Libena, Ifakara
27. Mhashamu Askofu Eusebius Nzigilwa, Dar es Salaam
28. Mhashamu Askofu Renatus Nkwande, Bunda
29. Mhashamu Askofu Gervas Nyaisonga, Mpanda /Dodoma
30. Mhashamu Askofu Bernadin Mfumbusa, Kondoa
31. Mhashamu Askofu John Ndimbo, Mbinga
32. Mhashamu Askofu Titus Mdoe, Dar es Salaam

No comments: