Sunday, July 12, 2009

Mambo ambayo wanaume

wanatakiwa kuyafahamu

kuhusu mwanamke




Imeandikwa na Halima Mlacha, Habari Leo


SUALA gumu katika uhusiano ni kutambuana tabia, pamoja na kwamba kila binadamu ameumbwa na tabia yake lakini kuna ukweli kuwa zipo tabia ambazo zinaendana kijinsia. Hapa namaanisha kuwa kuna tabia ambazo utakuta idadi kubwa ya wanawake au wanaume wanazo, hata kama hazifanani kabisa, angalau tabia hizo huendana na kumfanya mtu atambue kuwa hiyo ni jinsi ya kike au ya kiume.

Kwa pande zote mbili yaani wanawake na wanaume wamekuwa wakipata shida sana kutambua tabia halisi za jinsi nyingine hali inayowaletea ugumu na kuwafanya washindwe kutimiza kikamilifu lile wanalokusudia katika uhusiano walionao. Kwa leo nitazungumzia tabia ambazo ni za kawaida na hutokea mara kwa mara kwa wanawake hasa katika suala zima la mvuto katika uhusiano na tabia hizo ni tatu tu.

Wanawake mara nyingi huwa hawavutiwi na wanaume ambao hufanya vitendo vingi ili wapendwe au kuonekana na mvuto na wengi wa wanaume wanaopenda tabia hiyo hujikuta katika wakati mgumu. Upande mbaya wa tendo hilo la wanaume ni kwamba kwa baadhi yao hujikuta wakifanikiwa bila kutumia nguvu nyingi lakini pia wakiwa na hisia tofauti na zile za awali.

Wengi hao hujiona hawana mvuto katika jamii isipokuwa kile walichonacho na kwamba kama isingekuwa juhudi zake za kumvutia mwenza wake asingempenda au kukubali kuwa naye katika uhusiano. Lakini mbaya zaidi ni ugumu wao kutambua tatizo lao nini, hawafahamu nini cha kufanya au kipi cha kumvutia mwanamke, matokeo yake wanafikiri kumnunulia viti vya thamani au kumpa fedha ndio kunakomvutia, jambo ambalo linazidisha matatizo yao.

Napenda kuwakumbusha kuwa mvuto hauchagui, hakuna mtu anayeamua kuvutiwa tu na mtu na akavutiwa, mara nyingi mvuto hutokea tu hata wakati mwingine hujishangaa tunavutiwa na watu tusiowapenda kabisa, huo ndio mvuto. Na mara nyingi wanaume wanapojitahidi kufanya vitu ili kuwavutia wenza wao wa kike, hujikuta wakipata matokeo kinyume kabisa na matarajio yao.

Ni vigumu kwa wengi kuamini kuwa mwanamume anapomnunulia mwanamke zawadi, anapomweleza hisia zake siku ile tu waliyokutana naye na kumsifia kunaweza kumfanya mwanamke huyo akimbie. Cha kufanya ili kumfanya mwanamke avutiwe na mwanamume ni kwanza kuacha kumfuatafuata nyuma, jifunze namna ya kumfanya avutiwe na wewe, jifunze namna ya kutumiwa mbinu za mawasiliano ambazo zitamfanya awe na hisia na wewe.

Wanaume jifunzeni namna ya kuonyesha mapenzi yenu kwa wanawake mnaowapenda kwa kutumia maneno, vitendo, ishara na lugha ya mwili na utani. Kumfuata nyuma mwanamke na kumpigia simu kila saa kabla ya uhusiano wenu hakusaidii kunamkimbiza. Kumbukeni kuwa wanawake husoma kila kitu mwanamume anachofanya, bila kujali uzuri wa kitu chenyewe, kwa maana nyingine ni kwamba mara nyingi hutafsiri vitu hivyo kinyume.

Wanaume wao hupenda kuzungumzia kile kilicho kwenye mawazo yao na hukubaliana na kile wengine wanachokisema neno kwa neno, hapa ndipo wanapokuwa na matatizo na wanawake. Ninachoamini mimi ni kwamba wanaume wanao uwezo wa kuwasiliana na wanawake na kuwafanya wavutiwe nao, lakini tatizo ni kwamba bado hawajatambua uwezo wao huo na badala yake tamaduni, wazazi na lugha vimechangia kuficha uwezo huo.


dimbwimahaba@yahoo.com

au

dimbwimahaba@dailynews-tsn.com

1 comment:

Unknown said...

Nashukuru kwa kwa makala zako nzuri zina vutia zinapendeza sana ila sasa kama mmoja ndie anaonyesha upendo kwa mwenza vipi hapo maana ina wezekana unaonyesha upendo lakini mwenzio hayupo na wewe