Na Eeuteri Mangi na Hussein Makame - Maelezo
Rais wa Jamuhuri
ya watu wa China Xi Jinping anataraija kuanza ziara ya kihistoria nchini tangu
kuapishwa kwake kuitumikia nchi hiyo ambapo katika ziara
hiyo atasaini mikataba 17 ya ushirikiano wa kiuchumi kati ya
Serikali za Tanzania na nchi hiyo.
Akiongea na
waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa kimataifa Bernard Membe alisema kuwa ziara hiyo ni ya
kwanza barani Afrika kwa Rais huyo mpya wa China baada ya
kuchaguliwa kuliongoza taifa hilo Machi 14 mwaka huu.
Lengo la ziara
hiyo ambayo itaanza tarehe 24 hadi 25 Machi mwaka huu ni kukuza
uwekezaji na biashara baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania,Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa
China.
Baadhi ya Mikataba hiyo itahusiana na uboreshaji wa sekta ya viwanda, kilimo
hasa cha tumbaku ikiwemo kuwatafutia soko wakulima kutoka mikoa ya Tabora na
Ruvuma ili waweze kuuza zao hilo katika soko la China.
Waziri Membe alisema kuwa; “Mikataba mingine ni ya kulipatia Shirika la
Utangazaji Tanzania zana za kufanyia kazi na kuandaa mazingira ya ujenzi wa
bandari ya Bagamoyo itakayounganishwa na reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA),
reli ya kati na barabara”.
Rais Xi Jinping pia atazindua na kukabidhi rasmi kituo cha Mikutano
cha Kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere chenye ghorofa
tatu na kumbi nne za mikutano zenye uwezo kupokea washiriki
zaidi ya 1800 kilichogharimu dola za kimarekani milioni 29.7 zilizotolewa na
Serikali ya China kwa lengo la kumuenzi Mwalimu Nyerere.
Waziri huyo alisema kuwa baada ya kufika nchini Rais Xi Jinping atazungumza na
mwenyeji wake Rais Dk. Jakaya Kikwete pamoja na Viongozi Waandamizi wa Serikali
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na baadaye atahudhuria dhifa ya kitaifa
Ikulu Jijini Dar es salaam.
Siku ya pili ya ziara yake Rais Jinping atazungumza rasmi na Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk Ali Mohamed Shein pamoja
na ujumbe wa viongozi waandamizi kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Waziri Membe aliongeza kuwa Rais Jinping atatoa hotuba maalumu kwa Tanzania,
Afrika na Dunia kwa ujumla na kuzungumzia sera ya Serikali mpya ya China
kwa bara la Afrika ambayo itahudhuriwa na watu kutoka kada mbalimbali ikiwemo
Viongozi na Maafisa Waandamizi wa Serikali, Wahadhiri wa Vyuo Vikuu,Wabunge,
Viongozi wa Dini na Asasi za Kiraia na Wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali.
“Hotuba hiyo ya Rais wa China ataitoa kwa lugha ya Kichina na
kutafsiriwa kwa lugha ya Kiingereza na Kiswahili ili iweze kuifika
dunia nzima, hivyo tunaviomba vyombo vya habari nchini vichukue fursa hiyo kuwa
vya kwanza kuutangazia Ulimwengu” alisema Waziri Membe.
Ziara hiyo ya Rais
wa Jamhuri ya Watu wa China ni muendelezo wa uhusiano mzuri kati ya
nchi hiyo na Tanzania ulioasisiwa na viongozi wa mataifa hayo
mawili, yaani Mao Zedong wa China na Mwalimu Julius Nyerere wa
Tanzania.
Rais Jinping ataondoka nchini Machi 25 saa 10:40 jioni kuelekea nchini Afrika
Kusini kuhudhuria mkutano wa tano wa Wakuu wa Nchi zinazokuwa kwa kasi kiuchumi
ambazo ni Brazil, Urusi, India, China na Afrika ya Kusini (BRICS).
No comments:
Post a Comment